Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Thursday, September 11, 2014

SOMA HAPA !! Nimegundua njia za kulima bila kuwa na shamba ....Profesa Aboud!


Watu wengi katika jamii za mijini wameshindwa kuendesha shughuli za kilimo kwa kukosa ardhi. Hata hivyo, kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia ya kilimo kukua, hivi sasa inawezekana kuendesha shughuli za kilimo bila ya kutegemea ardhi au shamba kama ilivyozoeleka.
Ndiyo kusema kwamba hakuna haja ya watu wa mijini kutegemea mboga za sokoni kwani inawezekana kila mtu kuwa na kilimo hiki kisichotegemea ardhi nyumbani kwake. Mbali ya mtu kuepukana na kutegemea mboga za sokoni ambazo nyingi si salama kutokana na mazingira zinakolimwa na kuandaliwa, kilimo hiki pia kinaweza kumtoa mtu kimaisha kwa kuweza kujiajiri mwenyewe.
Tatizo kubwa ni kwamba watu wengi wa mijini hawana ujuzi na taaluma ya aina hii ya kilimo ambayo kitaalamu inaitwa ‘Aquaponics Agriculture’.
Aquaponics ni mfumo wa kuzalisha chakula ambao unajumuisha kilimo na ufugaji wa aina mbalimbali za samaki katika matenki na upandikizaji au ukuzaji mimea katika maji.
Kutokana na tatizo hilo Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro (MUM) kupitia Kitengo cha Kukuza Ujuzi kimeanzisha mafunzo maalumu ya kilimo hicho kwa vitendo. Kupitia mradi huo, chuo kinafanya mafunzo hayo yanayoratibiwa na Mtaalamu elekezi kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) Profesa Ali Aboud.
Profesa Aboud anasema kupitia aquaponics mtu anaweza kulima aina mbalimbali za mboga na vyakula kama nyanya, chinese na mchicha pamoja na aina mbalimbali za samaki wakiwamo perege na kambare.
Anasema kilimo hiki ni rahisi na chenye tija na kinaweza kumkomboa mjasiriamali au mkazi wa miji mikubwa ambayo kuna shida ya kupata ardhi za kuendesha shughuli za kilimo.
Profesa Abood anasema jambo la kwanza katika kuendesha kilimo hicho kinachojumuisha mifugo ya samaki ni kutengeneza mfumo wa maji utakaoruhusu maji hayo kuzunguka kutoka katika matangi ya maji yenye samaki, matenki yaliyopandwa mboga hadi katika tenki la kuhifadhia maji lililozikwa ardhini.
Anasema ili mfumo huo ukamilike unahitaji matangi ya maji ambayo yatakatwa juu ili kuruhusu mporomoko mzuri wa maji, mota inayotumia umeme kwa ajili ya kusukumia maji, mabomba kwa ajili ya kuunganisha mfumo wa maji, kokoto kwa ajili ya kuweka katika matenki yatakayopandwa mbogamboga na maji kulingana na ukubwa wa matangi.
“Ukishakamilisha mfumo wa maji unachohitaji ni kununua vifaranga vya samaki na kuvitumbukiza katika matangi ya maji na kutayarisha miche ya mboga unayotaka kuotesha na kuipanda katika matangi yenye kokoto,” anasema Profesa Abood.
Profesa Aboud anasema kuwa, mtu anaweza kujifunza ujuzi huu kwa muda siku tatu hadi tano na kuweza kuufanyia kazi vizuri.
“Lakini mwanafunzi au mtu anayehitaji ujuzi huu lazima pia tumpatie elimu ya msingi ya ufundi bomba”, anasema na kuongeza: “Katika kilimo hiki kinachojumuisha na ufugaji wa samaki, mkulima hahitaji mbolea, bali kinyesi cha samaki na mabaki ya vyakula vya samaki ndio vinakwenda kurutubisha mboga zilizopandwa, lakini kwa kile kisichojumuisha samaki kuna virutubisho maalumu lazima viwekwe.”
Kila mnyanya mmoja utazalisha angalau kilogramu 15 hadi 20 kwa muda wa miezi mitatu ya mavuno. Hivyo kilogramu 15 ukizidisha kwa idadi ya minyanya 64 utapata jumla ya kilogramu 960 kwa miezi mitatu.
Lakini kama utavuna kilogramu 20 kila mnyanya maana yake ni kwamba unazidisha 20 kilogramu mara 64 idadi ya minyanya yote ambapo utapata jumla ya kilogramu 1,280 ambayo ni zaidi ya tani moja.” anasema Profesa Aboud.
Kwa upande wa mavuno ya samaki, Profesa Abood anasema katika matenki mawili meupe yanayoonekana pichani wameweka vifaranga 70 vya perege kwa kila tangi.
“Tumefanya hivyo tukijua kwamba kuna wengine watakufa lakini baada ya miezi minne mpaka minne na nusu kila tangi tutavuna angalau kilo 35 za samaki, ambapo kwa matangi mawili tutavuna kilo 70 za samaki huku kila samaki mmoja akivunwa na uzito nusu kilogramu,” anasema na kuongeza:
“Hivyo kwa mwaka kila tangi litazalisha kilo mia moja za samaki kwa mavuno matatu.
“Hata kama unakaa karibu na bahari huwezi kula kilo 200 za samaki, lakini ukifuga unaweza kula tena kwa gharama nafuu. Unaweza kutumia kwa mboga nyumbani au hata kwa biashara.”
Profesa Aboud anafafanua kuwa, kilimo na mifugo ya aina hii ni mzuri kwa watu wa mijini kwani kinaweza kufanywa katika korido, uwani, barazani, uwanjani au hata kwenye sehemu ya juu ya jengo la ghorofa ‘top floor’.
Profesa Aboud anasema kama mtu hana fedha za kumwezesha kujenga mfumo wa maji ambao utamwezesha kulima na kufuga samaki, anaweza kulima tu kwa kutumia hata machupa ya maji, ndoo, makopo na vyombo vingine vya plastiki.
Akitolea mfano chupa la lita 10 la maji ambalo limeshatumika, anasema unalikata karibu na shingo yake, baada ya hapo kipande cha chini unaweka maji, cha juu unapanda mmea wa mboga unayotaka na kujazia kokoto na baadaye unaliweka juu ya kipande cha chini huku mizizi ya mmea huo ikizama ndani ya maji.
M'nchi

No comments:

Post a Comment